Mbona Basi Mnaifanya Migumu Mioyo Yenu?

“Mbona, basi mnaifanya migumu mioyo yenu, kama vile wale Wamisri, naye yule Farao, walivyoifanya mioyo yao?...” 1Samweli 6:6


Bwana Yesu Kristo asifiwe!

Ni jambo jema kumshukuru Mungu kwa kutupa kibali tena cha kuiona siku hii nyingine na wiki nyingine tena ya leo. Namshukuru mungu kwa wema na fadhili zake zinazotufuata siku zote za maisha yetu kila iitwapo leo.

Leo ningependa kuongea na wewe ambaye umekuwa unafanya moyo wako kuwa mgumu na hutaki kuisikia sauti ya Mungu na kumpa Yesu maisha yako. Naongea pia na wewe ambaye umeanguka dhambini na umeshindwa kurudi kwa Yesu tena.

Mbona unaufanya moyo wako kuwa mgumu? Mbona utaki kuokoka? Nini kinakuzuia kumpa Yesu maisha yako? Je ni mali au shughuli za dunia? Je ni wazazi, ndugu au mpenzi? Je unajiona bado wewe ni mdogo na unasema ngoja nile ujana kwanza, Yesu badae? Je dhambi zimekuzidia unaona kwamba huwezi kuziacha? Sijui sababu yako ni ipi ndugu yangu inayokufanya usimpe Yesu maisha yako.

Wakati ni sasa wa kumpokea Yesu na wala hakuna wakati mwingine, usiseme kesho kwa sababu hakuna aliye na uwakika na kesho.

Nisikilize ndugu yangu Yesu anakupenda sana. Laiti ungejua usingefanya moyo wako kuwa mgumu kabisa. Alikufa pale msalabani kwa ajili ya dhambi zako. Aliteseka kwa ajili yako. Upendo wake kwako hauna kipimo. Ni upendo ambao kwa akili za kibinadamu huwezi kuelezea.

Kwa maana jinsi hii Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele.” Yohana 3:16

Usiache upendo huu ambao Yesu anao kwako kukupita bure. Usikubali kuendelea kuteseka na dhambi, wakati yupo ambaye amekufa ili wewe upone.

Wewe ambaye umeanguka kwenye dhambi, mbona unaufanya moyo wako kuwa mgumu? Unasuburi nini kurudi tena kwa Yesu? Hata kama umeanguka zaidi ya mara moja, Yesu yupo tayari kukupokea tena. Tubu na urudi kwake. Nje uko kuna mbwa mwitu wakali, rudi kunduni mwa kondoo, usikubali kuendelea kuwa mtumwa wa hiyo dhambi?

Mungu anabisha kwenye mlango wa moyo wako anataka kukuokoa, anataka kukusaidia, anataka kukuponya, anataka kukupa uzima wa milele, anataka kukutoa kwenye utumwa wa dhambi, anataka kukupa amani na furaha ya kweli. Je uko tayari kumpokea?

Tazama, nasimama mlangoni, nabisha; mtu akiisikia sauti yangu, na kuufungua mlango, nitaingia kwake, nami nitakula pamoja naye, na yeye pamoja nami.”  Ufunuo wa Yonana 3:20


UFALME WA MUNGU UMEKARIBIA. USISEME KESHO KWA SABABU KESHO HUJUI UTAKUWA WAPI. WAKATI NI SASA. YESU ANAKUPENDA. MPOKEE YESU LEO ABADIRISHE MAISHA YAKO.

Maoni

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

Maamuzi Magumu (Wakoma Kishindo Cha Jeshi Kubwa)

Endelea Mbele (Bwana Atakupigania, Nawe Utanyamaza Kimya)

Wewe Ni Raia Wa Mbinguni