Maamuzi Magumu (Wakoma Kishindo Cha Jeshi Kubwa)

“Basi walikuwako watu wanne wenye ukoma, penye lango la mji; wakasemezana, Mbona tunakaa hapa hata tufe? Tukisema, tutaingia mjini, mjini mna njaa, nasi tutakufa humo; nasi tukikaa hapa, tutakufa vile vile. Haya! Twende tukaliendee jeshi la Washami; wakituhifadhi hai tutaishi; wakituua, tutakufa tu.” 2Wafalme 7: 3-4

Bwana Yesu asifiwe!

Namshukuru Mungu kipekee kabisa kwa kutupa neema ya kuiona siku hii mpya ya leo. Ni huruma zake tu kwamba hatuangamii. Fadhili zake ni mpya kila inapoitwa leo.

Leo Mungu ametupa tujifunze kuchukua maamuzi magumu. Maamuzi magumu waliyoyachukua wakoma hawa yaliwaokoa wao na Israeli yote kutoka kwenye njaa kali. Kama hawa wakoma wasingefanya maamuzi magumu kwa kuangalia hali walizonazo sijui kama chakula kingepatikana.

Walichukua maamuzi ambayo yalihatarisha maisha yao. Walikuwa tayari kupoteza maisha yao kwa sababu walijua hata kama wangebaki pale walipo wangekufa tu. Walichukua maamuzi ya kufa na kupona na kupitia maamuzi yao Israeli yote ilipona kutoka kwenye njaa kali.

Na kwa kuwa walikuwa tayari kuthubutu na kuchukua maamuzi magumu, Mungu alitumia miguu yao na kuzifanya ziwe kishindo cha jesi kubwa na washami wakapata hofu kuu na kukimbia na kuacha vitu vingi vikiwemo vyakula na mali kwenye kambi yao.

Tunajifunza nini kutokana na maamuzi magumu waliyochukua wakoma hawa wanne?

Mungu hahitaji mtu mwenye nguvu nyingi au akili nyingi au mtu maarufu ili afanye kazi yake. Mungu anahitaji mtu ambaye atasema mimi hapa Bwana nitumie. Haijalishi uwezo wake alionao. Anahitaji mtu anayeweza kufanya maamuzi magumu bila kuangalia hali alizonazo.

Mungu aliwatumia wenye ukoma kufukuza jeshi la washami. Mungu anaweza kukutumia wewe kufanya mambo makubwa bila kujali au kuangalia udhaifu wako. Anachohitaji ni wewe kufanya maamuzi magumu bila kuangalia hali uliyonayo.

Hawa watu wanne wangeweza kusema sisi hatuwezi bana tuna ukoma, tukae tu hapa tufe hamna haja ya kujisumbua. Lakini walichukua maamuzi magumua bila kuangalia hali waliyonayo na kupitia kwao waliliokoa taifa zima la Israeli.

Inawezekana unasema hali ni mbaya siwezi kufanya maamuzi. Kuna vitu ukiviona kwenye maisha yako unaona kama vinakuwa sababu ya wewe kutokuchukua maamuzi. Kumbuka hali uliyonayo sio sababu ya wewe kutokuchukua maamuzi.

Nani amekwambia Mungu anataka mtu aliyekamilika? Nani amekwambia Mungu anataka mtu mwenye hekima au akili nyingi? Nani amekwambia? Unachelewa kuchukua hatua leo ya kufanya jambo hilo kwa sababu unaona udhaifu ulionao.

Familia yako inawezekana inapitia kipindi kigumu kwa sababu ya wewe kutokuchukua maamuzi magumu. Inawezaekana hata taifa linapitia kipindi fulani kigumu kwa sababu tu kuna watu wachache walitega kusimama kwenye nafasi zao na kuchukua maamuzi magumu kwenye mambo fulani.

Ni bora ukachukua hatua leo hata kama utakosea kuliko kuendelea kukaa hapo tu bila kufanya kitu chochote. Kama wakoma wangeendelae kukaa pale hakika wangekufa na unajua hata taifa la Israeli lingeendelea kubaki na njaa kali na watu wengi wangekufa. Mungu ashukuriwe kwamba hawa jamaa walikuwa tayari kufanya maamuzi ya kufa na kupona na kwa sababu hiyo wakapona wao na taifa lao.

“Basi wakaondoka kabla ya mapambazuko, ili waende mpaka kituo cha Washami; walipofika mwanzo wa kimo cha Washami, kumbe! Hapana watu. Kwa maana Bwana alikuwa amewasikizisha Washami KISHINDO CHA FARASI, KAMA KISHINDO CHA JESHI KUBWA; wakaambiana, Tazama, mfalme wa Israeli amewaajiri wafalme wa Wahiti, na wafalme wa Wamsiri, waje wapigane nasi.” 2 Wafalme 7: 5-6

Wewe ni kishindo cha jeshi kubwa. Unaweza kufanya makubwa kama utaamua kuchukua hatua leo. Wale wakoma inawezekana wangejidharau na kusema sisi hatuwezi, lakini walipoamua, Mungu aliwatumia kama kishindo cha jeshi kubwa.

Nikomee hapa kwa leo. Tukutane tena kesho.

UNASUBIRI NINI KUOKOKA NA KUMTUMIKIA MUNGU? WAKATI NI SASA. MPOKEE YESU AWE BWANA NA MWOKOZI WA MAISHA YAKO. YEYE NDIO NJIA, KWELI NA UZIMA.


Maoni

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

Endelea Mbele (Bwana Atakupigania, Nawe Utanyamaza Kimya)

Wewe Ni Raia Wa Mbinguni